Mkurugenzi
wa ASET, Asha Baraka akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya
kuingia makubaliano na kampuni ya Proin Promotions Ltd ya kutengeneza
kazi zao kwa ubora zaidi. Kampuni hiyo tayari imetengeneza DVD ambazo
huwezi kunakili kwa lengo la kupambana na wezi wa kazi za wasanii. kulia
ni Meneja Masoko wa kampuni hiyo, Evans Steven na Afisa Mauzo, Kaisi
Masoud.
========= ======== =========
BENDI
ya muziki wa dansi nchini ya African Stars 'Twanga Pepeta', wameingia
mkataba maalumu na kampuni ya Proin Promotions Limited kwa ajili ya
utengenezaji wa kazi zao.
Akizungumza
na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Twanga Pepeta,
Asha Baraka, alisema mkataba huo una manufaa kwa bendi hiyo kutokana na
kutaka kuwanufaisha wanamuziki na wasanii wa nchini kwa ujumla.
Baraka
alisema kampuni hiyo ambayo awali ilikuwa ikijishughulisha na
usambazaji wa kazi za filamu, imeamua kuingia mkataba na bendi yake
kutokana na ubora wao.
Alisema
wasanii nchini wanatakiwa kunufaika na kazi wanayoifanya, na Prain
wameihakikishia Twanga kuwa kazi zao sasa zimetengenezwa kwa ubora wa
hali ya juu kiasi cha kumshinda mtu yeyote kuirudufu.
"Tunataka
maendeleo ya wasanii, tumekuwa tukiwakumbatia zaidi wasanii wa nje,
lakini muunganiko wetu sasa utasaidia kuinua hali ya kipato sahihi kwa
wanamuziki tulionao," alisema Baraka.
Kwa
upande wake, Ofisa Masoko wa Prain Promotions, Evance Steven, alisema
kampuni yao imeamua kuingia kwenye muziki na kuichagua Twanga Pepeta
kuwa bendi ya kwanza kutokana na kazi yao wanayofanya katika burudani.
Steven
alisema kazi kubwa waliyoanza nayo katika albamu ya Twanga Pepeta ya
Dunia Daraja ni kuhakikisha kuwa haiwezi kunakiliwa (kurudufiwa) upya na
maharamia wa kazi za kisanii nchini kama ilivyozoeleka.
"Tumewahakikishia
wenzetu wa Twanga Pepeta kuwa kazi zao sasa ziko salama kuuzwa kihalali
kutokana na kuziwekea programu maalumu ya kushindwa kunakilika, hivyo
kila mtu atanunua kihalali kazi za bendi hii za Dunia Daraja," alisema
ofisa huyo.
Twanga
itaanza kuuza kazi hizo katika kila maonesho yao huku zikionekana
kufungwa katika ubora wa hali ya juu alipokuwa akiwaonesha waandishi wa
habari utofauti mkubwa uliofanywa na Proin, ambapo pia zina stika
maalumu za TRA (Mamlaka ya Mapato Tanzania).
Comments