BALOZI WA TANZANIA RWANDA AWATEMBELEA AZAM FC NA KUWAAMBIA WAJITUME WAREJEE NA KOMBE DAR



Na Mahmoud Zubeiry, KIGALI
KAIMU Balozi wa Tanzania nchini Rwanda, Francis Aaron Mwaipaja amewataka wachezaji wa Azam FC kujituma na kuhakikisha wanachukua Kombe la Kagame, katika michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, michuano inayoendelea mjini hapa.
Balozi huyo amewatembelea wachezaji hao mchana katika hoteli waliyofikia, Kigali View mjini hapa na kuwapa hamasa waweze kufanya vizuri kwenye mashindano hayo.
Balozi Mwaipaja amesema kwamba amekuwa akizisikia sifa za Azam FC nchini Tanzania namna ambavyo imefuta utawala wa vigogo Simba na Yanga SC, hivyo anaamini ni timu nzuri.
Kombe liende nyumbani; Kaimu Balozi wa Tanzania nchini Rwanda, Francis Aaron Mwaipaja (katikati) akizungumza na wachezaji wa Azam FC leo
Kutoka kulia Leonel Saint-Preux, Ismaila Diara na Didier Kavumbangu wakimsikiliza Balozi

“Kitu cha msingi nataka niwaambie kwamba msifanye dharau, chezeni kwa kiwango kile kile dhidi ya kila timu muweze kushinda na kubeba Kombe, ili Tanzania ipate sifa kupitia nyinyi,”amesema.
Balozi amewasistiza wachezaji wa Azam kuelekeza nguvu na fikra zao kwenye mashindano yao ili wapeperushe vyema bendera ya Tanzania.
Nahodha wa Azam FC, John Raphael Bocco ‘Adebayor’ akizungumza kwa niaba ya wachezaji amemuahidi Balozi Mwaipaja kwamba watapigana kwa nguvu zao zote kuhakikisha wanabeba Kombe.
Meneja wa Azam FC, Jemadari Said pamoja kocha Mcameroon, Joseph Marius Omog nao pia wameungana na Nahodha Bocco kumuahidi Balozi taji.
Mabingwa hao wa Tanzania Bara, kesho watacheza mechi yao ya mwisho ya Kundi A Kombe la Kagame dhidi ya Adama City ya Ethiopia ingawa watamkosa beki aliye katika kiwango cha juu hivi sasa, Shomary Kapombe.
Mchezaji huyo wa zamani wa AS Cannes ya Ufaransa na Simba SC ya Tanzania pia, anasumbuliwa na nyama za paja na siku ya pili leo ameshindwa kufanya mazoezi na wenzake.
Kocha Omog ameiambia BIN ZUBEIRY leo kwamba, mbali na Kapombe, mshambuliaji Mhaiti pia Leonel Saint- Preux naye atakosekana- wote wakiwa wanasumbuliwa na maumivu ya nyama za paja.
Wachezaji wakimsikiliza Balozi leo
Kocha Joseph Omog kushoto akiteta na Msaidizi wake, Ibrahim Shikanda 

Beki Waziri Salum anasumbuliwa na maumivu ya kifundo cha mguu wakati kiungo Himid Mao ana kadi mbili za njano naye hatacheza.   
Nahodha Bocco ‘Adebayor’ aliyekosa mechi ya sare ya 2-2 na Atlabara ya Sudan Kusini, amefanya mazoezi jana na leo- maana yake kesho anaweza kurudi uwanjani.
Azam FC inahitaji ushindi kesho ili kuongoza Kundi A iweze kupata mpinzani nafuu katika Robo Fainali. Wenyeji Rayon Sport ambao watamaliza na Atlabara wanaongoza kundi hilo kwa sasa kwa pointi zao saba, wakati Azam ina pointi tano.
Atlabara yenye pointi tatu na Adama pointi mbili, zote zinataka kushinda kesho Uwanja wa Nyamirambo ili kuchukua nafasi ya tatu katika kundi hilo, ziweze kuungana na Azam na Rayon kwenda Robo Fainali. 

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA