Jumuia ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) imeishukuru na kuipongeza tena Tanzania kwa mchango wake mkubwa na wa hali na mali uliofanikisha jitihada za mapambano ya ukombozi yaliyoleta uhuru kwa nchi za Kusini mwa Afrika.
*Aidha, SADC yashukuru na kumpongeza Mzee Hashim Mbita.
Jumuia ya Maendeleo
Kusini mwa Afrika (SADC) imeishukuru na kuipongeza tena Tanzania kwa mchango
wake mkubwa na wa hali na mali uliofanikisha jitihada za mapambano ya ukombozi
yaliyoleta uhuru kwa nchi za Kusini mwa Afrika.
Aidha, SADC imemshukuru
na kumpongeza aliyekuwa Katibu Mtendaji wa Kamati ya Ukombozi ya Afrika,
Brigedia Hashim Mbita wa Tanzania, kwa mchango wake na uongozi wake wa
mapambano ya ukombozi, iwe katika nyanja ya kuviwezesha vyama vya ukombozi kwa
hali na mali, raslimali na ushauri.
Pongezi hizo kwa
Tanzania zilitolewa usiku wa jana, Jumamosi, Agosti 16, 2014, na Kikao cha
Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC – SADC Troika- kilichofanyika
kwenye Hoteli ya Elephant Hills Resort, Victoria Falls, Zimbabwe, chini ya
Uenyekiti wa Rais Hifikepunye Phohaba wa Namibia.
Mkutano huo wa SADC
Troika ulihudhuriwa na wanachama wa Asasi hiyo – nchi za Namibia, Lesotho na
Tanzania. Nchi za Afrika Kusini, Madagascar na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo
(DRC) zilishiriki kama waalikwa maalum wa kikao hicho.
Akizungumza kwenye
mkutano huo kwa niaba ya nwenzake, Rais Pohamba alisema: “Tunawashukuru wananchi wa
Tanzania kwa mchango wao wa kiuchumi, kijeshi na kimkakati katika kuunga mkono
kwa hali na mali jitihada za mapambano ya ukombozi wa nchi zetu.”
Aliongeza Rais Pohamba: “Sote
tunaijua Tanzania, sote tunawajua Watanzania.
Kwa pamoja walitoa jasho na damu na sisi wenyewe katika kutafuta ukombozi
wa nchi zetu. Tutaendelea kukumbuka na kuenzi mchango wao mkubwa na
usiosahaulika kwa ustawi wa nchi zetu.”
Kuhusu Mzee Mbita,
ambaye Ripoti yake ya shughuli za ukombozi ilitarajiwa kuwasilishwa kwenye
Mkutano wa Wakuu wa Nchi Wanachama wa SADC, Rais Pohamba alisema: “Brigedia
Mbita alifanya kazi mchana na usiku kufanikisha shughuli za ukombozi wa Kusini
mwa Afrika. Tunamshukuru sana kwa uongozi wake na mchango wake mkubwa katika
kuleta uhuru wa nchi zetu.”
Aliongeza: “Brigedia
Mbita ni raia wa Tanzania na alikuwa Katibu Mtendaji wa Kamati ya Ukombozi
Kusini mwa Afrika iliyokuwa na makao makuu yake mjini Dar es Salaam. Alichapa
kazi kweli kweli na chini ya uongozi wake, vyama vya ukombozi vilipata misaada
ya hali na mali, misaada ya kiroho na ushauri wa kijeshi kwa sababu yeye
mwenyewe alikuwa mtu wa shughuli za jeshi.” Mzee Mbita aliongoza Kamati
ya Ukombozi tokea mwaka 1974 hadi ilipomaliza shughuli zake.
Akizungumza kwa ufupi
sana katika kikao hicho, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa
Jakaya Mrisho Kikwete alimpongeza sana Brigedia Mbita akisema kuwa alifanya
kazi nzuri na kubwa na “tunampogeza kwa kazi nzuri sana ya kuandaa
Ripoti hiyo.”
Ripoti hiyo
inayojulikana kama Mradi wa Hashim Mbita iliongozwa na Meneja wa Mradi, Profesa
Arnold Temu wa Tanzania na imechapishwa na Kampuni ya Mkuki na Nyota, pia ya
Tanzania, ambayo Mtendaji Mkuu wake, Mzee Walter Bgoya ameandamana na
mwakilishi wa Mzee Mbita kwenye mkutano huo.
Imetolewa na;
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu – Dar es Salaam.
17 Agosti,2014
Comments