Mahakama
ya Mkoa,Vuga imempatia dhamana aliekuwa waziri wa zamani wa serikali ya
Mapinduzi (SMZ),Mansour Yussuf Himid anaetuhumiwa kwa kosa la kumiliki
silaha kinyume na sheria ya Zanzibar, baada ya kupata maelekezo kutoka
Mahakama kuu.
Hakimu
Khamis Ramadhani ametoa dhamana hiyo leo baada ya kutakiwa kusimamia
maamuzi ya kupatiwa dhamana yaliyotolewa na Mahakama kuu chini ya Jaji
Abraham Mwampashe kufuatia kusikilizwa kwa ombi la dhamana
lililowasilishwa Mahakamani hapo na mawakili wanaomtetea Mh.Mansour.
Mapema Jaji Abraham Mwampashe, akitoa dhamana hiyo, amesema Mahakama
yake imeangalia hoja za kisheria zilizotolewa na pande zote mbili za
muombaji na mpigaji dhamana zilizowasilishwa Mahakamani hapo na Mawakili
wa pande zote mbili.
Jaji Mwampashe amesema kutokana na kifungu cha sheria cha (150) kifungu
kidogo cha nne(4) sheria No (7 )ya mwaka (2004) sheria ya
Zanzibar,kinaipa uwezo Mahakama kuu kutoa dhamana kwa mtuhumiwa ikiwa
itaridhika na hoja zilizowasilishwa.
“Hakuna kosa lolote lisilokuwa na dhamana, kifungu kidogo cha nne (4)
kiko wazi kimeeleza Mahakama kuu ina uwezo wa kutengua makosa yote
yaliyokuwa hayana dhamana ikiwa itajiridhisha kama yalivyoorodhesha
katika kifungu kidogo cha kwanza” Alisema Mwampashe.
Amesema baada ya kuangalia hoja za kisheria pia ameangalia faida na hasara za mtuhumiwa kuwepo nje na kuwepo kizuizini.
Amesema gharama za kumhudumia na kumleta Mahakamani mtuhumiwa kunaitia
hasara jamii ,hivyo Mahakama hiyo haioni sababu ya mtuhumiwa kuendelea
kubaki kizuizini.
Mwampashe amesema hasa akiangalia mtuhumiwa hana historia ya uhalifu,pia
mtuhumiwa anamajukumu ya kuendesha biashara zake ambazo kunafaida ya
ajira kwa vijana walioajiriwa hapo katika vitega uchumi vyake.
Amesema Mahakama hii haiwezi kumyima mtu dhamana bila ya kuambiwa sababu
ya msingi kuwepo kwake nje kuweza kuathiri mwenendo mzima wa kesi yake.
Pia amefahamisha kwamba endapo Mahakama kuu itamnyima mtuhumiwa
dhamana,huku kesi inaendelea na kufikia kufutwa au mtuhumiwa kushinda
kesi, jamii inayomzunguka wataingia hasara ikiwemo kukosa huduma muhimu
kutoka kwa ndugu wanaemtegemea.
Aidha Jaji Mwampashe ametowa masharti ya dhamana kwa mtuhumiwa huyo
kutoa dhamana ya shilingi milioni tatu tasilim za Tanzania, wadhamini
wawili wanaoaminika kwa kusaini dhamana ya milioni tano za maandishi,
kwa kila mmoja.
Pia mtuhumiwa huyo alitakiwa kukabidhi Mahakamani hapo hati zake za
kusafiria, pia hatoruhisiwa kutoka nje ya Nchi bila ya kuiarifu
Mahakama.
Wakati huo, huo Hakimu Khamis Ramadhani alighairisha kesi mama
inayomkabili mtuhumiwa huyo hadi Agosti 28,mwaka huu na mtuhumiwa yuko
nje baada ya kutimiza masharti yote ya dhamana.
Taarifa na Hamed Mazrui kupitia facebook
Comments