Waziri
wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dkt. Seif Rashidi akiwasha moja ya kati
ya magari manne aliyoyapokea kutoka kwa mwakilishi wa shirika la
GLRA la Ujerumani nchini Burchard Rwamtoga leo jijini Dar es salaam.
Mwakilishi
wa shirika la GLRA nchini Burchard Rwamtoga (kushoto) akimkabidhi
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dkt. Seif Rashidi (kulia) ufunguo
wa moja kati ya pikipiki 20 zilizotolewa na shirika la hilo leo
jijini Dar es salaam.
SERIKALI
kupitia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imepokea msaada wa gari 4
na pikipiki 20 vyenye thamani ya Tsh. Milioni 261 kutoka Shirika la
GLRA kutoka nchini Ujerumani kwa ajili ya kusaidia mapambano ya
ugonjwa wa Kifua Kikuu na Ukoma nchini.
Mikoa
ambayo imenufaika na msaada huo ni pamoja na Tanga, Kigoma, na Mikoa
ya Kanda Maalum ya Ilala na Kinondoni.
Akipokea
msaada huo leo (Jumanne Agosti 26, 2014) Waziri wa Afya na Ustawi wa
Jamii, Dkt. Seif Rashidi (Mb) aliwataka Waganga Wakuu wa Mikoa na
Wilaya kusimamia kikamilifu matumizi ya vyombo hivyo vya usafiri kwa
kuvilinda na kuvitumia kulingana na malengo yaliyokusudiwa.
Dkt.
Seif alisema kuwa vifaa hivyo vimegawiwa kulingana na mgawanyo wa
mikoa iliyoanishwa na Serikali katika Mpango wa Taifa wa kudhibiti
ugonjwa wa kifua kikuu na ukoma.
Dkt.
Seif alisema Mpango wa Taifa wa kudhibiti kifua kikuu na ukoma
umekuwa na mafanikio ambapo imeendelea kutoa matibabu kwa wagonjwa
wote wa kifua kikuu na ukoma bila malipo katika hospitali na vituo
vya huduma za afya vya serikali na binafsi nchini.
Aidha,
Dkt. Seif amesema kuwa Tanzania imevuka malengo ya Shirika la Afya
Duniani (WHO) kwa kuponyesha asilimia 85 ya wagonjwa wote wa kifua
kikuu wanaoanza matibabu kila mwaka.
“Takwimu
zinaonesha kuwa Tanzania imefikia viwango vya asilimia 88 ya
kuwahudumia na kuwaponyesha wagonjwa hao ambayo ni zaidi ya kiwango
cha WHO” alisema Dkt Seif.
Dkt.
Seif amesema kuwa kwa upande wa ugonjwa wa ukoma, Serikali inaendelea
kufanya kampeni katika mikoa ya Dar es salaam, Dodoma, Kagera, Lindi,
Morogoro, Mwanza, Pwani, Rukwa, Shinyanga, Tabora na Tanga katika
kutoa elimu kwa wananchi namna ya kujikinga na ugonjwa huo.
Kwa
mujibu wa Dkt. Seif alisema wagonjwa wapya wa ukoma waliogunduliwa
mpaka sasa na kupatiwa tiba ni 23,667, na Serikali tayari imetoa jozi
35,000 ya viatu maalumu kwa wagonjwa hao.
“Mpaka
sasa tumeweza kufikia malengo ya kimataifa ya kutokomeza ukoma kwa
kuwa chini ya mgonjwa mmoja katika watu 10,000 na kufanya ugonjwa wa
ukoma kuwa si tatizo kubwa la kiafya kwa jamii nchini” alisema Dkt
Rashid.
Naye
mwakilishi wa shirika lisilo la kiserikali la GLRA nchini Burchard
Rwamtoga aliusifu kwa ushirikiano uliodumu kwa miaka 37 baina ya
Shirika hilo na Serikali ya Tanzania katika mapambano ya magonjwa ya
ukoma na kifua kikuu.
Aidha,
Rwamtoga aliongeza kuwa Shirika la GLRA hutoa wastani wa Tsh. Bilioni
1.3 kila mwaka kwa Serikali na kati ya fedha hizo kiasi cha
Tsh.milioni 600 hutumika kwa ajili ya manunuzi ya vifaa vya
usafirishaji ikiwemo magari, na pikipiki kwa waratibu wa kifua kikuu
na ukoma.
GLRA
mbali na kutoa fedha kwa Serikali pia tunaratibu mpango wa
kuwajengea uwezo wa kiutendaji waratibu wa mikoa ikiwemo kutoa
mafunzo nje ya nchi kupitia kituo cha ALERT kilichopo nchini
Ethiopia, ambacho hujisihusha na mafunzo ya upasuaji na kutoa
visaidizi ikiwamo miguu bandia na baiskeli kwa wagonjwa.
Kwa
upande wake Mratibu wa huduma za kifua kikuu na ukoma mkoa wa Ilala
Dkt. Mbarouk Seif ameishukuru Serikali kuupatia mkoa huowake gari la
wagonjwa na kuahidi kuwa Ofisi yake itahakikisha gari hilo
linawafikia na kuwahudumia wagonjwa kwa wakati.
Shirika
la GLRA ilianza kusaidia wagonjwa wa ukoma nchini mwaka 1959 na
kupata usajili mwaka 1977 ambapo lilianza kushirikiana na Mpango wa
Kudhibiti kifua kikuu na ukoma (NTLP) nchini uliopo chini ya Wizara
ya Afya na Usatawi wa Jamii.
na fredy mgunda
Comments