SITTA; BUNGE LA KATIBA HALITOVUNJWA KAMWE



WAKATI baadhi ya wanaharakati wakishinikiza Bunge Maalumu la Katiba liahirishwe Mwenyekiti wake, Samuel Sitta (pichani) amesema kamwe halitavunjwa ili kuokoa fedha za wananchi zilizotumika.

Kutokana na hilo alisema kuwa kuahirishwa kwa Bunge hilo, hatua ambayo hata hivyo pamoja na kuwa kumekuwepo na shinikizo kubwa kutaka hatua hiyo ichukuliwe, haitawezekana kwa mujibu wa sheria.

Sitta alisema hayo jana ofisini kwake bungeni mjini hapa wakati alipokutana na ujumbe kutoka Mfuko wa Vyombo vya Habari Tanzania (TMF) ulioambatana na baadhi ya wanahbari wa vyombo mbalimbali.

Alisema anashangaa wanaoshinikiza liahirishwe jambo ambalo litakuwa ni sawa na kuteketeza fedha za wananchi kwa vile mchakato ulianza muda mrefu zaidi ikilinganishwa na muda uliobaki.

Sitta ambaye pia ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki alisema vikao vya Bunge hilo vinaendelea kufanyika kihalali kama sheria inavyobainisha na kuwa lingeweza kusitishwa kama wajumbe wa kundi moja wangetoka wote.

Alisema kuwa makundi yote yote yapo na yanahudhuria vikao vya kamati yakiwemo Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na kundi la 201 huku akisisitiza kuwa yeye anaaamini Katiba itakayopatikana itakuwa bora.

Mwenyekiti huyo, alionesha kutoridhishwa na kutokuwepo kwa uwazi katika uendeshaji wa Serikali, hali ambayo inasababisha wanahabari hapa nchini kupata wakati mgumu katika utendaji wao.

Kwa upande mwingine alisema wamepokea mapendekezo ya Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) kuhusu Baraza la Habari kuingizwa katika Rasimu ambayo inaendelea kujadiliwa na wajumbe kupitia kamati zao.

Wakati hayo yakijiri, wajumbe wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) wakikosekana katika kamati mbalimbali kwenye Bunge la Katiba linaloendelea, Mwenyekiti wa Kamati namba 8, Job Nduga amesema akidi inatosha.

Alisema katika kamati yake Mjumbe, John Shibuda ambaye ni miongoni mwa wajumbe sita wa Ukawa anaendelea kushirikiana na kamati hiyo yenye jumla ya wajumbe 52 inayokutana kupitia sura mbalimbali za Rasimu.

Ndugai ambaye pia ni Naibu Spika alibainisha kuwa wajumbe wenzake wanaendelea na majadiliano kwa maelewano na wameweza kupiga kura kwa utaratibu mzuri ingaa kumekuwa na mgongano wa hoja.

Suala la uraia wa nchi mbili yaani uraia pacha kwa mara nyingine limetikitisa Bunge Maalumu hususan katika kamati hiyo namba 8 huku wanaopendekeza suala hilo wakishutumiwa kwa kukosa uzalendo.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA