Wadau mbalimbali wa madini ya vito waliopata bahati kutembelea Banda la Tanzania katika siku ya kwanza ya Maonesho ya 54 ya Kimataifa ya Vito na Usonara ya Bangkok, wakishangazwa na mng’ao wa Kito cha Tanzanite katika Pete iliyovalishwa kidoleni mwa Mwanafunzi, Raia wa Thailand aliyeomba kujaribisha Pete hiyo. Anayetoa maelezo ni Mfanyabiashara wa Madini ya Vito kutoka Tanzania, Bw. Gregory Kibusi (Mwenye mavazi ya Bhatiki).
Pic
2
Mkurugenzi wa Kitengo
cha Uthaminishaji wa Madini ya Almasi na Vito cha Wizara ya Nishati na Madini
(TANSORT), Archard Kalugendo akizungumza na mdau wa madini ya vito
aliyetembelea Banda la Tanzania. Kalugendo alitumia fursa hiyo kumkaribisha
mdau huyo katika Maonesho ya Vito ya Arusha yanayotarajiwa kufanyika mwezi Septemba
mwaka huu nchini Tanzania. Katikati ni Afisa kutoka Wizara ya Nishati na
Madini, Asimwe Kafrika.
Sehemu ya shehena ya madini mbalimbali ya vito katika Banda la Tanzania kwenye Maonesho ya 54 ya Kimataifa ya Vito na Usonara ya Bangkok.
Wafanyabiashara wa
Madini ya Vito kutoka Tanzania, Gregory Kibusi (Mwenye nguo za Bhatiki) na
Kassim Iddi Pazi (Mwenye Shati la rangi ya Bluu), wakimwonyesha Mteja aina
mbalimbali za madini ya vito yanayopatikana Tanzania.
Mgeni Rasmi katika
ufunguzi wa Maonesho ya 54 ya Kimataifa ya Vito na Usonara ya Bangkok, ambaye
ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Biashara ya Thailand, Bi. Chutima Bunyapraphasara,
akikata utepe kuzindua rasmi Maonesho hayo. Kushoto kwake ni Rais wa Taasisi ya
Wafanyabiashara wa Madini ya Vito wa Thailand, Bw. Somchai Phornchindarak na
Kulia kwake ni Mkurugenzi Mtendaji wa Idara ya Uhamasishaji Biashara Kimataifa,
Bibi Nuntawan Sakuntanaga.
Baadhi ya Viongozi
kutoka Taasisi na Mashirika mbalimbali ya kiserikali na binafsi yanayoshiriki
katika Maonesho ya 54 ya Kimataifa ya Vito na Usonara ya Bangkok, wakiwa katika
picha ya pamoja na Mgeni Rasmi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Biashara ya Thailand,
Bi. Chutima Bunyapraphasara (katikati – mwenye sketi ndefu).
Mkurugenzi wa Kitengo
cha Uthaminishaji wa Madini ya Almasi na Vito cha Wizara ya Nishati na Madini -
Tanzania (TANSORT), Archard Kalugendo (wa kwanza kushoto) akiwa katika picha ya
pamoja na Kamati iliyoandaa maonesho husika.
Na
Veronica Simba - Bangkok
Banda la Tanzania
katika siku ya kwanza ya Maonesho ya 54 ya Kimataifa ya Vito na Usonara ya
Bangkok, yaliyozinduliwa Septemba 9, 2014 nchini Thailand, limekuwa na mvuto wa
kipekee kwa wadau wa madini husika kutoka mataifa mbalimbali duniani waliofika
katika maonesho hayo.
Mkuu wa Banda la
Tanzania, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kitengo cha Uthaminishaji wa Madini ya
Almasi na Vito cha Wizara ya Nishati na Madini (TANSORT), Archard Kalugendo alisema,
wadau wengi waliofika katika maonesho hayo, walivutwa na aina mbalimbali za
madini ya vito yanayopatikana Tanzania hususan Tanzanite.
“Unajua, Tanzanite ni
madini yanayopatikana Tanzania pekee ambapo sifa hii inayafanya kuwa madini
yenye mvuto wa pekee,” alisema Kalugendo.
Aliongeza kuwa, mbali
na kuwa Tanzanite inapatikana Tanzania pekee, lakini pia ina mvuto wa pekee
machoni mwa watazamaji ambayo ni sababu nyingine inayowavutia watu wengi
kupenda kufahamu zaidi kuhusu madini hayo, hali ambayo imesababisha watu wengi
kutembelea Banda la Tanzania.
Alifafanua kuwa,
pamoja na kuwepo mabanda kutoka nchi nyingine yaliyo na madini ya Tanzanite
katika maonesho hayo, wengi wa wadau
walitembelea Banda la Tanzania wakitaka kuelimishwa zaidi kuhusu madini hayo,
hali inayodhihirisha kuwa ufahamu kwamba Tanzanite inatoka Tanzania pekee
umeongezeka kwa watu kutoka mataifa mbalimbali.
Wakizungumza kwa
nyakati tofauti, Wafanyabiashara wa Madini ya Vito kutoka Tanzania wanaoshiriki
katika maonesho hayo, Gregory Kibusi na Kassim Pazi walisema ushiriki wa
Tanzania katika maonesho husika kwa msimu huu umeboreka zaidi kutokana na
maandalizi mazuri yaliyofanyika.
“Tulitumia uzoefu
tulioupata katika maonesho ya msimu uliopita na hivyo tukajipanga vizuri zaidi
kuhakikisha tunakuwa na ushiriki wenye tija msimu huu na ndiyo maana katika
siku ya kwanza tu ya maonesho, tumeshuhudia banda letu likitembelewa na watu
wengi sana,” alisema Kibusi.
Naye Gregory
alifafanua kuwa maandalizi waliyofanya ni pamoja na kuandaa madini ya kutosha
hasa yale yaliyokatwa tayari, ambayo ndiyo yanayopendwa zaidi na wadau wengi
wanaofika katika maonesho.
Kwa upande wake,
Mtaalamu wa Madini ya Vito kutoka TANSORT, ambao ndiyo waratibu na wasimamizi
wa ushiriki wa Tanzania katika maonesho hayo, Teddy Goliama alisema maandalizi
mengine yaliyofanyika ni pamoja na kuwepo na washiriki wengi zaidi wakijumuisha
wachimbaji na wafanyabiashara wa madini husika pamoja na maafisa kutoka
Wizarani.
Vilevile alisema
kuwa, mbali na kutangaza madini mbalimbali yaliyopo Tanzania, Ujumbe wa
Tanzania unaoshiriki katika maonesho hayo unafanya kazi ya kuitangaza nchi kwa
ujumla ikiwa ni pamoja na fursa mbalimbali za uwekezaji pamoja na vivutio vya
utalii.
“Tumeamua kutumia
fursa hii ya maonesho kuitangaza nchi kwa ujumla. Tunawashukuru Wizara ya
Maliasili na Utalii kupitia Bodi ya Utalii ambao walitupatia vipeperushi, picha
za video na makabrasha mbalimbali yenye kutangaza vivutio vya utalii wa nchi
yetu. Tumegawa vipeperushi vingi ambavyo tunaamini vitasaidia sana kuitangaza
nchi yetu katika anga za kimataifa na hivyo kuvutia watalii na wawekezaji wengi
zaidi,” alisema Teddy.
Maonesho ya 54 ya
Kimataifa ya Vito na Usonara ya Bangkok, yaliyofunguliwa Septemba 9 mwaka huu
na Katibu Mkuu wa Wizara ya Biashara ya Thailand, Bi. Chutima Bunyapraphasara,
yanatarajiwa kuhitimishwa Septemba 13, 2014. Hii ni mara ya pili kwa Tanzania
kushiriki maonesho hayo.
---mwisho---
Imeandikwa
Septemba 10, 2014.
Comments