*Ni wa kujenga maghala makubwa ya kuhifadhia chakula
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amesema
Serikali inaangalia uwezekano wa kupata mkopo wenye masharti nafuu
kutoka Serikali ya Poland utakaoliongezea Taifa uwezo wa kuhifadhi
chakula tofauti na hali ilivyo sasa.
Alisema uzalishaji mwaka huu
umetoa ziada ya tani milioni 1.5 za nafaka na tani 800,000 za mpunga
ikilinganishwa na ziada ya tani 300,000 iliyokuwepo mwaka jana.
“Serikali inakabiliwa na changamoto ya kupata soko la uhakika kwa mazao
ya wakulima kwa sababu tulizoea kumtumia Wakala wa Hifadhi ya Taifa ya
Chakula (NFRA) kama mnununzi mkuu na uwezo wezo wake ni tani 240,000 tu
kwa mwaka,” alisema.
Akizungumza baada ya kutembelea
kampuni ya MLYNPOL ambayo inanunua mazao kwa wakulima na kusindika
nafaka jana mchana (Ijumaa, Oktoba 24, 2014) Waziri Mkuu alisema
teknolojia ya ujenzi wa maghala makubwa ya kuhifadhia chakula katika
muda mfupi ndiyo suluhisho pekee kwa wakulima wa Tanzania katika kipindi
tulichonacho.
“Wenzetu wana teknolojia ya kisasa
ya ujenzi wa SILOS (maghala makubwa ya kuhifadhia chakula) pamoja na
namna bora ya kuhifadhi chakula, na sisi tuna changamoto ya kuwasadia
wakulima kuuza mazao kutokana na uzalishaji mkubwa wa nafaka ambao
umetokea mwaka huu,” alisema.
Alisema ni mapema mno kujua kiasi
cha fedha ambacho Serikali inatarajia kukopa lakini alithibitisha kwamba
atatuma timu ya wataalamu kutoka sekta husika ili wafanye mazungumzo
rasmi na Serikali ya Poland na kukamilisha taratibu za upatikanaji wa
mkopo huo.
Waziri Mkuu ambaye alisafiri km.
500 kwenda mji wa CHOJNOW kilipo kiwanda cha kutengeneza maghala (SILOS)
na kusindika nafaka aliguswa na teknolojia inayotumika kwenye kiwanda
hicho cha MLYNPOL ambapo kwa siku moja kina uwezo wa kusindika tani
360,000.
Mji wa CHOJNOW upo kusini
Mashariki mwa Poland na pia hauko mbali na mipaka ya nchi za Ujerumani,
Czeck na Austria. Kwa gari dogo ni kati ya saa 3 hadi 4 hadi kufika miji
mkuu ya nchi hizo ambayo ni Berlin, Prague na Vienna.
Akitoa maelezo kwa Waziri Mkuu,
mmiliki wa kiwanda hicho kikubwa nchini Poland, Bw. WITOLD KARCZEWSKI
alisema kiwanda hicho kinaposindika ngano kina uwezo wa kutoa unga laini
wa mikate (refined flour), unga wa lishe (grain/brown flour), unga wa
kutengeneza pasta na tambi na wa mwisho hutolewa kwa ajili ya chakula
cha mifugo.
“Nafaka zikifika, zinasafishwa,
zinakaushwa, zinapimwa unyevunyevu uliopo na kuanza kusindikwa kulingana
na aina ya nafaka inayoletwa. Tunakusanya mazao haya kutoka kwa
wakulima kwenye majimbo 16 ya nchi hii,” alisema.
Akifafanua kuhusu matumiai ya
umeme kwenye kiwanda hicho, Bw. ALEKSANDR ZINGMAN ambaye pia ni mshauri
na mbia wa Bw. KARCZEWSKI, alisema kiwanda hicho kinatumia megawati moja
ya umeme kwa saa moja lakini matumizi yanaweza kupungua kuligana na
ukubwa ama udogo wa kiwanda.
“Kama Serikali inahitaji kiwanda kidogo zaidi ya hapa, tunaweza kuwajengea na matumizi ya umeme lazima yatapungua,” alisema.
Kampuni ya MLYNPOL ina wafanyakazi 250 ambao kato yao, 200 wanafanya kazi kiwandani kwa shifti tatu za saa nane nane kila moja.
Waziri Mkuu anamalizia ziara yake
ya siku tatu nchini Poland jana mchana ambapo asubuhi alikutana na
Watanzania waishio Poland na baadaye kufanya vikao na baadhi ya
wafanyabiashara wa jiji la Warsaw.
Comments