Utata wajitokeza kifo cha Meshack Yebei




Hali tata imezidi kujitokeza juu ya kifo cha Meshack Yebei, anayetajwa kuwa shahidi katika kesi inayomkabili Naibu Rais wa Kenya William Ruto.
Shahidi huyo alitarajiwa kutoa ushahidi katika mahakama ya kimataifa ya uhalifu-ICC dhidi ya naibu Rais wa Kenya.
Lakini mwishoni mwa wiki mwili wa Yebei ambao ulionekana kuunguzwa kiasi ,ulikutwa umetupwa kando ya mto huko Eldoret Magharibi mwa nchi hiyo
Familia ya Yebei wanashuku kwamba chanzo cha mauaji hayo ilikuwa ni kumzuia ndugu yao asiweze kutoa ushahidi wake katika mahakama ya ICC huko The Hague.
Hata hivyo msemaji wa mahakama ya kimataifa ya uhalifu wa kivita, ICC Fadi El Abdallah ameiambia BBC kuwa Bwana Yebei hakuwa katika orodha ya mashahidi rasmi wa upande wa mashitaka katika mahakama ya ICC.
Amesema, kuna makundi tofauti ya watu wanaoweza kupewa ulinzi na mahakama ya ICC, ambao ni pamoja na makundi tofauti ya mashahidi wawe ni wale wa upande wa mashitaka, utetezi na majaji au wawakilishi wa waathirika na zaidi ya hapo ICC inaweza kutoa ulinzi kwa watu wengine binafsi au kwa sababu ya kuwa na uhusiano na ICC lakini bila kuwa mashahidi rasmi. "Na katika hatua hii kile tunachoweza kueleza ni kuwa Bwana Yebei hakuwa katika orodha ya mashahidi wa ICC upande wa mashitaka kinyume na kilichoripotiwa katika badhi ya vyombo vya habari.Lakini kwa minajiri ya uchunguzi hatuwezi kueleza yeye yuko katika kundi gani la watu wanaolindwa na ICC" amesema Bwana Fadi.
Mwendesha mashitaka mkuu wa ICC, Fatou Bensouda amewahi kunukuliwa akisema kuwa mashahidi kadha mpaka sasa wamekuwa wakitishiwa maisha na matokeo yake wengi wamejitoa katika ushahidi wa kesi hiyo iliyokuwa ikiwakabili viongozi kadha wa taifa la Kenya akiwemo Rais Uhuru Kenyatta ambaye hivi karibuni amefutiwa mashitaka na mwendesha mashitaka mkuu huyo wa ICC,kwa kile alichoeleza kuwa ni kukosekana kwa ushahidi ambao ungetosheleza kuendelea na kesi hiyo, baada ya mashahidi wengi kujitoa au kudaiwa kuuawa na hata kukosa vielelezo vingine ambavyo angevitumia kama ushahidi katika kesi hiyo.
Awali aliyekuwa mwendesha mashitaka mkuu wa ICC, Louis Ocampo aliwafungulia kesi watu sita, ambao alisema ni wahusika wakuu katika kesi ya ghasia za baada ya uchaguzi mkuu nchini Kenya 2007.
Watuhumiwa hao walikuwa ni pamoja na Uhuru Kenyatta, ambaye wakati huo alikuwa naibu waziri mkuu na waziri wa fedha, Francis Kirimi Muthaura, aliyekuwa katibu wa baraza la mawaziri,na Mohammed Hussein Ali, mkuu wa polisi wa zamani. Wengine ni Henry Kosgey, aliyekuwa waziri wa viwanda,William Ruto, aliyekuwa waziri wa elimu na baadaye kusimamishwa na Joshua Arap Sang, mtangazaji wa redio moja nchini Kenya.
Naibu Rais William Ruto na mtangazaji wa redio Joshua Arap Sang ndio waliobakia katika kesi hiyo ya ghasia za baada ya uchaguzi mkuu nchini Kenya ambapo watu wapatao 1,200 waliuawa na wengine 500, 000 kukosa.CHANZO:BBC

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI