WANANCHI MKURANGA WAASWA KUCHANGIA DAMU.

      

unnamedMkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Prof. Emanuel Mjema (kulia) akimkabidhi Mganga Mfawidhi wa hospitali ya wilaya ya Mkuranga Dkt. Anwar Milulu (kushoto) msaada wa mashuka yenye 90 yaliyotolewa na chuo hicho kusaidia wagonjwa katika hospitali hiyo.Makabidhiano hayo yalifanyika jana wilayani Mkuranga kama  sehemu ya Chuo hicho kuadhimisha miaka 50 toka kianzishwe mwaka 1965. unnamed1Baadhi ya Wauguzi na wahudumu wa afya wa hospitali ya wilaya ya Mkuranga wakiangalia moja ya shuka kati ya mashuka 90 yaliyotolewa na Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) kusaidia wagonjwa wanaolazwa katika hospitali hiyo. unnamed2Mkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Prof. Emanuel Mjema (katikati) akitoa ufafanuzi kuhusu msaada wa mashuka  90 yaliyotolewa na chuo hicho katika hospitali ya wilaya ya Mkuranga ikiwa ni sehemu ya mpango wa chuo hicho kutoa huduma kwa jamii.
unnamed4Baadhi ya viongozi wa Chuo cha Elimu ya Biashara CBE wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa hospitali ya wilaya ya Mkuranga jana.
……………………………………………………………………………..
Na. Aron Msigwa –MAELEZO.
 Mkuranga, Pwani.
Wananchi wilayani Mkuranga wametakiwa kujenga utamaduni wa kuchangia  damu kwenye  benki ya damu iliyoko katika hospitali ya wilaya hiyo ili kupunguza tatizo la uhaba wa damu linaloikabiri hospitali hiyo.
Kauli hiyo ilitolewa jana wilayani Mkuranga na Mganga Mfawidhi wa hospitali ya wilaya  hiyo, Dkt. Anwar Milulu wakati akipokea msaada wa mashuka 90 yaliyotolewa na Chuo cha Elimu ya Biashara Dar  es salaam (CBE) kwa lengo la kuwasaidia wagojwa wanaolazwa katika hospitali hiyo.
Alisema kuwa hospitali hiyo kwa sasa inakabiliwa na changamoto ya uhaba wa damu kutokana na mwamko mdogo wa wakazi wa wilaya hiyo wanaojitokeza kuchangia damu jambo linalosababisha upungufu wa damu na usumbufu kwa wagonjwa wanaohitaji kuongezewa damu .
“Kama mnavyoona hospitali yetu iko barabarani kwa sasa tunakabiliwa na tatizo la upungufu wa damu, baadhi ya wagonjwa hutufikia wakiwa katika hali mbaya  ya kuhitaji kuongezewa damu kiasi cha  kutufanya tuwapeleke katika hospitali ya Taifa Muhimbili  kuokoa maisha yao” Alisema Dkt. Milulu.
Alieleza kuwa lishe duni na kutozingatia ulaji wa mboga za majani kama inavyoshauriwa na wataalam wa afya ni miongoni mwa sababu zinazochangia kuendelea kwa tatizo la upungufu wa damu kwa akina mama wajawazito na watoto.
Dkt. Milulu alifafanua kuwa hospitali hiyo imekuwa ikitoa elimu kwa wagonjwa hususan akina mama wajazito na watoto pindi wanapohudhuria Kliniki kwa lengo la kuwaeleza umuhimu wa uzingatiaji wa lishe bora na namna ya  kukabiliana na tatizo la upungufu wa damu miongoni mwa jamii.
Aidha, alisema Serikali inaendelea kuyatafutia ufumbuzi matatizo ya ukosefu wa maji,uhaba wa miundombinu  na dawa yanayoikabili hospitali hiyo kutokana na idadi kubwa ya wagonjwa wa kawaida na wale walio katika makundi maalum wanaohudumiwa na hospitali hiyo ikilinganishwa na uwezo wake.
“Serikali inaendelea kushughulikia tatizo la maji,miundombinu na upungufu wa dawa unaoikabili hospitali yetu maana idadi ya wananchi tunaowahudumia ni wengi ikilinganishwa na uwezo wa miundombinu ya hospitali”
Kuhusu changamoto ya rasilimali watu na wataalam wa kada mbalimbali alisema kwa sasa hospitali hiyo  ina idadi inayoridhisha ya  Madaktari, Wauguzi, wahudumu, wataalam wa maabara na madereva ikilinganishwa na miaka iliyopita.
Alitoa wito kwa uongozi wa chuo hicho kuendelea kuisaidia hospitali hiyo katika masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuwahamasisha wanafunzi wa chuo cha CBE kujitokeza kuchangia damu mara kwa mara  ili  kuokoa maisha ya wagonjwa.
Nao baadhi ya wananchi waliokuwa wakipatiwa huduma katika hospitali hiyo wakizungumza kwa nyakati tofauti licha ya kuushukuru uongozi wa chuo cha CBE kwa kuwakumbuka kwa kuwapatia msaada wa mashuka hayo walikiri kuwepo kwa mwamko mdogo wa wananchi  kuchangia damu katika benki ya damu ya hosptali hiyo.
Aidha, waliiomba Serikali kulishughulikia tatizo la  maji , miundombinu na uhaba wa dawa uliopo katika hospitali hiyo na kuwaomba wadau wengine wajitokeze kuisaidia hospitali hiyo ili iweze kutoa huduma bora kwa wananchi.
Awali akizungumza msaada huo Mkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) Prof. Emanuel Mjema alisema kuwa chuo chake ifikapo Januri 21, 2015 Chuo cha  Elimu ya Biashara kinatimiza miaka 50 hivyo msaada walioutoa ni sehemu ya huduma kwa jamii.
Alisema katika kuelekea kutimiza  miaka 50 ya chuo cha CBE mbali na kujikita katika masuala ya kuelimisha jamii katika taaluma  mbalimbali ikiwemo Biashara, Ugavi na manunuzi, Vipimo, TEHAMA na Utawala katika biashara kimekua kikitoa huduma mbalimbali kwa jamii.
Alisema katika kuelekea maadhimisho ya miaka 50 chuo hicho kimekuwa kikitoa misaada ya vitu mbalimbali na elimu ya ujasiriamali kwa wananchi katika mikoa yote ambayo kina matawi yake ikiwemo Dar es salaam, Mbeya, Zanzibar, Mwanza na Dodoma.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*