Kmanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Leonard Paul akionesha baadhi ya vifaa vya mlipuko vilivyokamatwa na watuhumiwa 10 waliokutwa wamejificha ndani ya Msikiti Ruaha, wilayani Kilombero, Morogoro jana. Baadhi ya vifaa vilivyokamatwa ni sare za jeshi, majambia, bendera nyeusi na bunduki. (PICHA ZOTE NA PETER KIMATI)
WATU 10 wanaotuhumiwa kujiandaa kufanya ugaidi wamekamatwa msikitini wakiwa na milipuko 30, sare za jeshi, bendera nyeusi pamoja na vitu mbalimbali vya kufanyia uhalifu huku mmoja akichomwa moto na wananchi wenye hasira katika tarafa ya Kidadu wilayani Kilombero.
Kamanda wa polisi mkoa wa Morogoro,Leonald Paul alimesema tukio hilo limetokea Aprili 14 mwaka huu saa 3.30 usiku katika kitongoji cha Nyandero, tarafa ya Kidadu wilayani Kilombero.
Kamanda Paulo alimtaja aliyefariki katika tukio hilo ni Hamad Makwendo mkazi wa Manyasini Ruaha wilayani Kilombero, ambaye ndiye anadaiwa kuwa mwenyeji wa watuhumiwa hao wengine kumi waliotiwa mbaroni na jeshi hilo
Alisema siku ya tukio jeshi la polisi walipata taarifa za watu hao za kujihusisha na uhalifu na kuanza kufuatilia kwa muda na ambapo walikuta watu hao tayari walishaondoka na kuelekea maeneo yasiyojulikana.
Alisema polisi walipata taarifa kuwa watu hao walitumia usafiri wa bajaji mbili, ambao wakati wakiendelea na zoezi la kufutilia ndipo walikutana na bajaji moja ikiwa na abiria mmoja na hivyo kuisimamisha bajaji hiyo
Alisema bajaji hiyo iliposimama ndipo Hamadi ambaye ni marehemu aliruka na kuanza kukimbia, askari mwenye namba F .3323 koplo Nasoro alianza kumkimbiza na alipomkaribia mtuhumiwa huyo alichomoa jambia na kumkata askari huyo shingoni na kuvuja damu nyingi
Alisema askari mwingine mwenye namba E9245 koplo Chomola ambaye alikuwa nyuma alifanikiwa kumpiga risasi ya mguu mtuhumiwa huyo, alipoanguka chini wananchi wenye hasira walifika eneo hilo na kuanza kumshambulia marehemu huyo kisha kumchoma moto mpaka mauti
Hata hivyo kamanda huyo alisema polisi iliwalazimu kuongeza kikosi cha polisi kutoka mkoani, waliendelea na zoezi la kuwasaka watu wengine ambapo walipata taarifa wako katika msikiti wa Suni uliopo Kidatu.
Alisema polisi hao walipofika katika msikiti huo waliomba viongozi wa msikiti kwa kushirikiana na viongozi wa serikali kuwatoa watu wote waliokuwa msikitini ili kuweza kubaini watu ambao wanatiliwa mashaka kuhusika na matukio ya kihalifu
Alisema waumini wote walitakiwa kutoka nje ya msikiti wakiwa na mabegi yao, na ndipo polisi walipoendesha zoezi la ukaguzi na kufanikiwa kuwakamata watu hao kumi wakiwa na vifaa mbalimbali vya kufanya uhalifu
Kamanda huyo alisema vitu vilivyokutwa katika mabegi hayo ni pamoja na milipuko 30, bendera nyeusi yenye maandishi ya Mungu mmoja, nyaya(detonators) , majambia , bisibisi, mask, nguo za jeshi, misumeno ya chuma, spana piperange, madaftari, vitabu mbalimbali vikiwemo vya risiti.
Kamanda huyo alisema mbali na vitu hivyo pia marehemu alikutwa na risasi sita tano za bunduki ya SMG na moja ya bunduki aina ya mark iv pamoja na detonators fuse mbili zikiwa katika mfuko mdogo wa jeshi.
Kamanda huyo alisema askari polisi huyo aliyejeruhiwa alitokwa damu nyingi na kwamba alikimbizwa katika hospitali ya kiwanda cha sukari cha Kilombero na hali yake inaendelea vizuri huku wakifanya utaratibu wa kumhamishia hospital ya mkoa wa morogoro
Comments