HOTUBA
YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA
TANZANIA,
MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE KWENYE SIKUKUU YA KUWEKWA WAKFU NA KUSIMIKWA
MHASHAMU
ASKOFU LIBERATUS SANGU,
KUWA
ASKOFU WA JIMBO KATOLIKI SHINYANGA,
TAREHE
12 APRILI, 2015
Mwadhama Polycarp
Kardinali Pengo;
Mhashamu Askofu Mkuu,
Tarsisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Tanzania;
Mheshimiwa Balozi wa
Vatican, Mhashamu Askofu Mkuu Protase Rugambwa;
Mhashamu Askofu Liberatus Sangu, Askofu Mpya wa Jimbo
Katoliki Shinyanga;
Wahashamu Maaskofu
Wakuu na Maaskofu;
Waheshimiwa Mawaziri
na Naibu Mawaziri;
Mheshimiwa Mkuu wa
Mkoa wa Shinyanga;
Viongozi wa Dini na Serikali
Mliohudhuria;
Ndugu Waumini,Wageni
Waalikwa;
Mabibi na Mabwana:
Tumsifu Yesu Kristo!
Shukrani na Pongezi
Napenda
kuungana na nyote mlionitangulia kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa rehema na baraka
zake zilizotuwezesha kushiriki pamoja katika tukio hili muhimu na adhimu kwa
Jimbo Katoliki Shinyanga kupata Askofu wake wa nne. Nawashukuru Baraza la
Maaskofu Katoliki Tanzania na Jimbo Katoliki Shinyanga kwa heshima kubwa mliyonipa
ya kunialika katika sherehe ya kuwekwa wakfu na kusimikwa Mhashamu Baba Askofu Liberatus
Sangu kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki Shinyanga. Hii ni heshima kubwa kwangu na
kwa Serikali yetu na ni kielelezo hai cha
uhusiano mzuri uliopo kati
ya Kanisa Katoliki na Serikali.
Mhashamu
Baba Askofu Liberatus Sangu;
Nakupongeza
kwa kuteuliwa kwako na kwa leo hii kukabidhiwa rasmi dhamana ya kuwa Kiongozi Mkuu
wa Jimbo Katoliki la Shinyanga. Uteuzi wako kushika wadhifa huu ni uthibitisho
wa imani kubwa aliyonayo Baba Mtakatifu Francis
kwako. Imani hiyo ndiyo pia waliyonayo
wajumbe wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, makasisi, watawa na walei wa
Jimbo la Shinyanga. Sote, tumeusubiri
uteuzi huu kwa hamu tangu tulipopata pigo la kuondokewa na mpendwa wetu Baba
Askofu Aloysius Balina mwaka 2012.
Nakuomba
utambue kuwa imani hiyo imebeba matumaini makubwa kwamba utaitenda kazi yako
kwa moyo wa dhati, uadilifu na uaminifu mkubwa. Kwa kawaida matumaini ya
waamini kwa kiongozi wao wa kiroho huwa makubwa na wakati mwingine huwafanya
wakasahau kuwa kiongozi wa dini pia ni binadamu. Lakini wanafanya hivyo kwa nia
njema na kwa sababu nzuri kwamba hakuna mwingine ila wewe. Mimi naamini kwamba kwa malezi mazuri uliyopatiwa
na Kanisa lako ukichanganya na uzoevu wako wa muda mrefu wa kazi za kichungaji,
uwanazuoni wako na kwa rehema za Mwenyezi Mungu utayamudu vyema majukumu yako
ya kuwaongoza kondoo wa Bwana kwenye malisho mazuri ya kiroho na kimwili.
Maadili Mema
Mhashamu
Baba Askofu Liberatus Sangu;
Waheshimiwa
Maaskofu;
Ndugu
Waumini na Wageni Waalikwa;
Malisho ya kiroho huwafanya waumini wawe wacha Mungu. Na, mcha
Mungu kwa kawaida humpenda Mungu na jirani yake, huzingatia maadili mema, huwa
na tabia njema na mara nyingi huwa raia mwema. Kwa ajili hiyo, viongozi wa dini
kama walivyo wa Serikali wanao wajibu maalum wa kulilea taifa. Ninyi mnalea kiroho, kwa maana ya kuwafanya waumini
kufuata taratibu za kiimani na sisi
tunalea kidunia kwa maana ya raia kufuata taratibu za kikatiba na kisheria na
maadili mema kwa mujibu wa mila na desturi za jamii na nchi yetu.
Ninyi viongozi wa dini
huwalea waumini kiimani waweze kutende mema hapa duniani ili waje kupata malipo
mazuri wanaporejea kwa Muumba wao. Hili
la kulea kiimani likifanikiwa basi kwa kiasi kikubwa kazi ya Serikali inakuwa rahisi.
Hapatakuwa na watu wanaoiba, wanaoua wenzao, wanaokata albino viungo vyao, wanaotukana
wenzao, matapeli, wanaofumaniwa na kadhalika. Hivyo basi, Serikali
ingepunguziwa kasi ya kuwakamata,
kuwafikisha mahakamani na kuwafunga magerezani watu wengi kama tufanyavyo sasa. Hivyo basi, mchango wenu katika kujenga
maadili mema kwa jamii na watu wake ni kitu kilicho bayana. Aidha, pale tunapokuwa na jamii iliyojaa
maovu, umuhimu na ukubwa wa kazi yenu unaonekana bayana. Napenda kutoa ombi maalumu kwako Baba Askofu
Sangu pamoja na Maaskofu, Mapadre katika mikoa ya kanda hii kuongeza bidii
katika kuelimisha jamii kuacha mauaji ya vikongwe na watu wenye ualbino. Tushirikiane na Serikali kupamba na
ushirikina kitu ambacho ndicho chanzo cha mauaji haya na kukatwa viungo
albino. Ninyi mnasikilizwa sana,
itumieni nafasi hiyo tuondokane na aibu hii.
Mchango wa Kanisa Katika Maendeleo ya Taifa
Waheshimiwa Maaskofu;
Uhusiano kati ya Serikali na madhehebu ya dini likiwemo Kanisa Katoliki
ni wa muda mrefu na ni wa kihistoria. Serikali imekuwa ikiunga mkono shughuli
za Kanisa katika kutoa huduma za jamii za elimu, afya na nyinginezo zenye kuwaletea
maendeleo wananchi. Mmetoa mchango mkubwa sana ambao umewanufaisha Watanzania
wengi wa dini na madhehebu mbalimbali. Huduma
hizi zimesaidia sana kuongeza kasi ya kuwatoa wananchi kwenye umaskini na kujiletea
maendeleo. Tunawapongeza na kuwashukuru
sana kwa mchango wenu mkubwa.
Haistaajabishi kuwa matumaini ya waamini wa Kanisa Katoliki, Jimbo
la Shinyanga na wananchi wa Shinyanga kwa ujumla juu yako Baba Askofu Sangu siyo
ya kiroho pekee. Wanatarajia kuwa chini ya uongozi wako, Kanisa Katoliki
litaendelea kutoa huduma za jamii kwao.
Wana matumaini hayo kwa sababu wanatambua na kuthamini manufaa makubwa
wanayopata katika harakati zao za kujiletea maendeleo kutokana na kazi njema
inayofanywa na Kanisa. Wanategemea utaendeleza kazi nzuri zilizofanywa na
waliokutangulia na utabuni na kutekeleza miradi mingine mipya ya maendeleo
katika Jimbo lako. Nami naungana nao na, sina mashaka juu ya usahihi wa imani
yao hiyo kwako.
Ahadi ya Serikali
Mheshimiwa Baba Askofu;
Napenda kukuhakikishia ushirikiano wangu binafsi na ule wa
Serikali ninayo iongoza katika kutekeleza majukumu yako ya kiroho na ya huduma
za kiuchumi na kijamii kwa maendeleo ya wananchi wa Shinyanga. Pale utakapo ona
mchango wa Serikali unahitajika, usisite kuwasiliana nasi. Na iwapo utaona kuna
upungufu wo wote sema kwa viongozi wa Wilaya, Mkoa na wa kitaifa: Waziri Mkuu, Makamu wa Rais na hata
kwangu. Sisi ni wasikivu. Tuite
tutakuitika. Ukituambia tutakujibu kwa lile linalohitaji majibu na tutatenda
kwa lile la kufanya, bora tu liwe kwenye uwezo wetu na ni wajibu wetu kufanya.
Wahashamu Maaskofu;
Sisi katika Serikali tunayo kila sababu ya kuendeleza uhusiano
mzuri kati yetu na madhehebu ya dini maana kazi muifanyayo haina badala yake. Tunaamini kwa dhati kuwa, kwa pamoja tunaweza
kujenga, kuimarisha na kuendeleza amani, umoja na mshikamano uliopo katika
taifa letu. Hali kadhalika, tukishirikiana tutaongeza kasi ya kuwawezesha
Watanzania kupata maendeleo.
Tutaendelea kutimiza wajibu wetu wa kutengeneza mazingira mazuri
kwa madhehebu ya dini kutekeleza majukumu yake.
Kuna mambo mawili: Jambo la kwanza ni kuhakikisha kuwa uhuru wa
kuabudu unakuwapo nchini, unaheshimiwa na unatekelezwa kwa vitendo. Hii ni haki inayotambulika na Katiba yetu ya
sasa na utekelezaji wake hauna kasoro. Bahati
nzuri imesisitizwa na kufafanuliwa vizuri zaidi katika Katiba Inayopendekezwa.
Pili, tutaendelea kushirikiana na
kusaidiana kwa upande wa shughuli zenu za huduma za kiuchumi na kijamii
mzifanyazo. Tumekuwa tunatoa misamaha ya
kodi kwa shughuli za madhehebu ya dini na hata kuchangia fedha za Serikali na
watumishi kwa baadhi ya shughuli zenu hasa za afya na mikopo ya wanafunzi
katika vyuo vikuu. Tutaendelea kufanya
hivyo kwa kutambua mchango muhimu unaotolewa na huduma hizo kwa maendeleo ya
nchi yetu na ustawi wa watu wake. Maombi
yangu au yetu kwenu ni kuwa msiwaruhusu watu waovu wakaitumia vibaya fursa hii
muhimu. Tunapopata taarifa za fursa hiyo
kutumika kinyume hutusumbua sana.
Tuendako
Mwadhama
Kardinali;
Waheshimiwa
Maaskofu;
Wageni
Waalikwa;
Wakati wote sisi viongozi wa Serikali na dini tunao wajibu wa kipekee
katika uhai wa taifa letu na watu wake.
Tunalo jukumu maalum la ulezi, yaani kuhakikisha watu katika nchi yetu
wanaishi kwa amani, umoja, upendo na
mshikamano licha ya tofauti zetu za rangi, kabila, dini, jinsia, maeneo
tutokako, au ufuasi wa vyama vya siasa.
Naomba tukumbuke kuwa tofauti hizi ambazo hatuna budi kuishi nazo, tusiziache zikawa nyufa za uhasama ambao siyo
tu zitaligawa taifa bali zinaweza kulimong’onyoa na kulisambaratisha.
Sisi viongozi tuna wajibu wa kihistoria wa kutambua kuwa ni jukumu
letu kuhakikisha kuwa hilo haliwi.
Nayasema haya kwa sababu. Kwa
jumla tunapita katika kipindi kisichokuwa cha kawaida, ambacho kama
hatutafanikiwa kubadili mwelekeo huu kunaweza kuwepo madhara makubwa. Nawaahidi
ushirikiano wangu binafsi na wa Serikali ninayoiongoza. Naomba viongozi wa dini msaidie ufa usiwe
mpana zaidi. Tumieni Kamati za dini kwa mwaka
kama huu wa uchaguzi ambapo baadhi ya
wanasiasa na washabiki wao katika tamaa yao ya kupata madaraka hupenda
kuzitumia tofauti hizi kwa maslahi yao binafsi na vyama vyao, tunaomba muwe
makini zaidi. Wakati mwingine wanasiasa hufanya
makusudi kuchochea uhasama kwa kutumia tofauti zetu za asili ili wapate manufaa
ya kisiasa. Wao hawajali inayoweza kutokea
na madhara makubwa kwa nchi yetu.
Kwa ajili hiyo, niwaombe viongozi wa dini tutumie vizuri nafasi ya uongozi mliyojaaliwa na Mwenyezi
Mungu kuzuia wanasiasa wasilifikishe taifa pabaya. Watakeni waumini wenu wasiwasikilize na
kufanya mambo yote yanayofarakanisha jamii bali washikilie yale yanayowaunganisha
na kuleta utangamano. Na lililo muhimu
kuliko yote ninalowaomba msiwape wanasiasa fursa kuingiza dini kwenye siasa au
siasa kwenye dini. Tuambieni bila
kigugumizi. Wasiziache dini ziwe huru
kwa watu wa vyama vyote. Makanisa na
Misikiti ibaki kuwa nyumba za ibada na siyo majukwaa ya siasa. Iwe mahali pa kuwaunganisha wote na viongozi
wa dini wawe kimbilio lao wakati wanapogombana.
Msikubali ufuasi wa vyama vya siasa ukawafarakanisha viongozi wa
dini mpaka mkapoteza dira na nafasi yenu muhimu ya uongozi wa waamini
wenu. Kuchanganya dini na siasa ni
hatari sana kwa usalama, amani na utulivu wa jamii na hata dini zenyewe. Si vyema wakati wa Chama cha siasa kushindwa kukawa
ni kushindwa dini fulani na waumini wake au Chama na kushinda ni kwa dini
nyingine na waumini wao. Wafuasi wa
vyama vya siasa kugombana si jambo la ajabu.
Je itakuwaje kama dini
zimehusishwa na kugawanyika kidini. Ugomvi
huo unakuwa na sura ya ugomvi baina ya wafuasi wa dini tofauti kwa mwamvuli wa
siasa? Kuna hatari ya kuzuka vita vya
kidini na nchi ikawaka moto. Kunaweza
kutokea maafa yasiyotabirika sura yake na mwisho wake. Naomba viongozi wa dini mtambue wajibu wenu
wa kuponya. Tuwaache waumini wawe
wafuasi wa vyama vya siasa wavipendavyo.
Kwa uchaguzi muwahimize waumini wenu wachague kwa busara kadri watakavyoridhishwa
na sera, ilani na ahadi za vyama vya siasa na wagombea wao. Wasisitizeni kujali ubora, moyo wa uzalendo
na uadilifu wa wagombea. Tukifanya hivyo
tutavuka salama. Kinyume chake inaweza
kuzua tatizo.
Hitimisho
Mheshimiwa
Baba Askofu;
Leo ni siku ya
furaha kwetu sote. Ni siku pia ya
kumsifu Mwenyezi Mungu kwa neema zake na kumshukuru kwa uteuzi wako. Waumini waliofurika hapa wamekuja kwa ajili
ya sherehe za kuwekwa wakfu na siyo Mkutano wa Rais. Niruhusu niishie hapa nitoe nafasi kwa
kuabudu na kumtukuza Mungu wetu.
Nitatafuta wasaa mwingine mwafaka wa kuzungumza na wananchi wa Shinyanga
na Watanzania kwa jumla kuhusu mambo ya maendeleo.
Nikushukuru tena kwa kunialika na kwa kunipa heshima hii ya
kuzungumza na viongozi wa Kanisa,
waumini na wananchi. Mwenyezi
Mungu na akubariki Baba Askofu na akufanyie wepesi katika majukumu yako.
Asanteni kwa
kunisikiliza.
Comments