Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete jana
Jumapili, Aprili 12, 2015 aliungana na maelfu ya waumini wa Kanisa Katoliki,
Jimbo la Shinyanga, kuhudhuria Ibada rasmi ya kumweka wakfu na kumsimika Askofu
mpya wa Jimbo hilo, Mhashamu Baba Askofu Liberatus Sangu.
Rais
Kikwete aliwasili kwenye Kanisa Kuu la Mama Mwenye Huruma, Ngokolo, mjini
Shinyanga kiasi cha saa sita unusu mchana kwa ajili ya Ibada hiyo
iliyohudhuriwa pia na Maaskofu wakuu, maaskofu na maaskofu wasaidizi 38,
akiwamo Askofu Mkuu wa Jimbo la Dar es Salaam Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo
na Rais wa Mabaraza ya Kipapa na Katibu Mwambata wa Uenezaji Injili Ulimwenguni
Askofu Mkuu Protase Rugambwa kutoka Makao Makuu ya Kanisa Katoliki, Vatican.
Askofu
Sangu ambaye amewekwa wakfu na kusimikwa kwenye Siku ya Huruma ya Mungu Duniani
anakuwa Askofu wa nne wa Jimbo la Shinyanga na anachukua nafasi iliyoachwa wazi
tokea Novemba 6, 2012, wakati aliyekuwa Askofu wa Jimbo hilo, Baba Askofu
Aloysius Balina alipofariki dunia.
Kwa
miaka karibu mitatu, jimbo hilo limekuwa chini ya Usimamizi wa Kitume wa Askofu
Mkuu Yuda Tadei R’uaichii wa Jimbo Kuu la Mwanza.
Askofu
Sangu mwenye umri wa miaka 52 baada ya kuwa amezaliwa Februari 19, Mwaka 1963,
katika Kijiji cha Mwazye, Jimbo Katoliki la Sumbawanga, Mkoa wa Rukwa, alipata
daraja la upadrisho Julai 3, Mwaka 1994. Wakati anateuliwa na Baba Mtakatifu
Francesco kuwa Askofu Februari 2, mwaka huu wa 2015, alikuwa na daraja la
Mosinyori.
Akikabidhi Jimbo hilo kwa Askofu mpya, Askofu
Mkuu R’uaichii amesema kuwa Jimbo la Shinyanga ni moja ya majimbo makubwa zaidi
ya Kanisa Katoliki nchini, likiwa na kilomita za mraba karibu 30,000 na waumini
Wakatoliki wanaokaridiwa kufikia 300,000 katika Mkoa ambao idadi kiasi ya
wakazi wake bado wanaamini imani za
jadi.
Amesema
kuwa Jimbo hilo lina parokia 29, mapadre wa Jimbo 52, mapadre wa Kitawa 18 na
hivyo kulifanya jimbo hilo kuwa na jumla ya mapadre 70 na “jeshi kubwa” la
watawa 70.
Kwenye
sherehe hizo zilizohudhuriwa na viongozi wengi wa Serikali akiwemo Mkuu wa Mkoa
wa Shinyanga, Mheshimiwa Ali Lufunga, Askofu Sangu amepewa zawadi ya sh.
milioni 18, fimbo ya kiuchungaji na ng’ombe 10 wa maziwa na Wakatoliki wa Jimbo
hilo.
Rais
Kikwete alirejea Dar es Salaam jana jioni baada ya kumalizika kwa Ibada hiyo.
Mwisho.
Imetolewa na;
Kurugenzi
ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu – Dar es
Salaam.
13
Aprili, 2015
Comments