NIMESHANGAZWA SANA NA HAWA WAARABU KUWA NA MBINU ZA KIZAMANI


Na Maulid Kitenge, Tunisia
WAKATI mpira ukiwa unabadilika duniani, Waarabu bado wamejaa kasumba ileile ya kizamani ya mambo ya ajabu kabla ya mchezo.


Niko mjini Tunis, Tunisia kwa ajili ya mechi ya marudiano ya Yanga na wenyeji wa hapa, Etoile du Sahel, itakayopigwa kesho usiku mjini Sousse lakini nilichokiona sikuamini. Nikajiuliza, hivi kwenye karne hii mambo haya ya fitna za Kiarabu bado yapo?

Kwanza wamewagandisha Yanga uwanja wa ndege kwa saa mbili, wakisema wanashughulikia viza lakini kilichokuwa kinafanyika kilikuwa hakionekani mpaka msafara wa Yanga ulipoamua kuchachamaa na kupiga kelele, ndipo wenyeji walipoharakisha kushughulikia suala la viza. Nikajiuliza hivi mpaka watu wapige kelele?


Timu kubwa kama Etoile du Sahel ambayo tayari ina rekodi ya aina yake barani Afrika ya kunyakua karibu makombe yote, sikutegemea kama itafanya ubabaishaji wa aina hiyo. Nilijua kama walikuwa wanafanya, basi zamani na siyo sasa.

Hivi dunia ya leo ukamgandishe mgeni wako uwanja wa ndege ‘airport’ ili umuondoe mchezoni!

Lakini kituko kingine kilikuja wakati timu ilipotoka uwanja wa ndege na kukumbana na gari lililoandaliwa na wenyeji hao, eti Toyota Coaster ambayo imechoka, kwamba hiyo ndiyo Yanga wafanye nayo safari ya saa moja na nusu kuelekea mjini Sousse ambako kutachezwa mchezo huo wa marudiano kesho Jumamosi.

Bahati nzuri kumbe Yanga walishajiandaa wakawa wamekodi basi kubwa na lile Toyota Coaster ambalo liliandaliwa kwa ajili ya wachezaji tukapanda akina sisi.

Wakati nikiwa nimekaa kwenye gari hilo lililochakaa, nilikuwa najiuliza; kumbe ndiyo maana Afrika tukienda Kombe la Dunia hatufiki mbali! Na kwa hali hii tunastahili tusifike mbali, maana bado kasumba za hujuma za kizamani tunazo wakati wenzetu Wazungu hawana mambo haya.

Sasa kama miamba Etoile wanafanya mambo kama haya, timu ndogo za Afrika nazo zitajifunza nini? Nilichojifunza ni kwamba sisi Watanzania tumekuwa wakarimu sana. Ipo haja sasa nasi kufanya mambo kama haya kwa vile timu zetu ugenini zinafanyiwa.

Siku zote Watanzania, klabu hata za Waarabu zinapokuja kucheza soka nchini, huwa tunazikarimu sana wakati sisi tukienda kwao tunafanyiwa vitendo vya ajabuajabu.

Kama tunataka kushindana nao, basi angalau japo kwa muda tuwe na sisi tunauweka ubinadamu kando ili tuwachanganye kama wanavyotuchanganya sisi. Tuwaondoe mchezoni kama wao wanavyotuondoa sisi mchezoni.

Kama tusipofanya kama wao wanavyotufanyia, bila shaka hatuwezi kushindana nao na kuwatoa, kwa kuwa wao wanaweza wasituzidi uwezo uwanjani, bali wanatuzidi hujuma za nje ya uwanja.

Lakini kwa namna yoyote ile, mambo kama haya tunapaswa kuyakemea kwa kuwa yanaua soka letu. Nchi za Afrika haziwezi kufanya vizuri katika mashindano ya Kombe la Dunia kwa kuwa zinategemea sana hujuma, kitu ambacho siyo sawa.

Kwa kuwa Waarabu hawataki kusikia, basi nasi tuzibe masikio kwa pamba, tukikutana nao basi iwe jino kwa jino ili tuende nao sawa.

Vinginevyo tutakuwa tukitupwa nje ya michuano tukikutana nao wakati pengine uwezo wa uwanjani tunao, tena kuliko hata wao.


SOURCE: CHAMPIONI

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI